HomeResourcesSabbath School quarterly

Jinsi ya Kujifunza Biblia

25/04/2026

Somo la Juma Hili

Yohana 15:1-8; Marko 1:35; 1 Nyakati 16:11; Zaburi 119:105; Isaya 50:4; Isaya 55:1–13.

Fungu la Kukariri

"Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma" (#Isaya 55:11#).

Hebu kumbuka siku ulipopokea Biblia yako ya kwanza. Pengine ulikuwa mtoto na ulipewa na ndugu aliye Mkristo. Au pengine uliinunua mwenyewe ukiwa mtu mzima. Iwe umekuwa na Biblia yako kwa muda mrefu kiasi gani (pengine sasa una zaidi ya nakala moja), tafakari juu ya thamani unayokipatia Kitabu hiki. Je, ni moja kati ya vitu vyako vyenye thamani zaidi, au unachukulia kirahisi kwamba unalijua sana Neno la Mungu? Je, una wakati mgumu katika kuwa thabiti katika ratiba ya kulisoma? Je, umepata kujiuliza: Ninapaswa kuanzia wapi? Nisomeje Kitabu hiki ili niweze kuwa karibu zaidi na Mungu?

Martin Luther alisema, “Kwa miaka kadhaa nimekuwa nikisoma Biblia yote mara mbili kila mwaka. Kama Biblia ingekuwa ni mti mkubwa sana na maneno yake yote yangekuwa matawi madogo madogo, ningekuwa nimegonga matawi yote, nikiwa na shauku ya kujua kilichokuwa pale na kile ambacho Biblia ingekitoa.”

Uwe unapitia uzoefu wa kusisimua wakati wa kujifunza Biblia, au ikiwa Biblia yako hukaa muda mrefu zaidi ikiwa imefungwa kwenye safu ya vitabu ukweli ni kwamba sisi sote tunaweza kujenga nyakati bora zaidi kujifunza Biblia pamoja na Mungu. Juma hili tutaangalia baadhi ya njia za kivitendo za kujifunza Neno la Mungu kwa namna iliyo bora zaidi.

Jifunze somo la juma hili kwa maandalizi ya Sabato ya Mei 2.